TANI 9 ZA DAWA ZA KULEVYA ZAKAMATWA NCHINI, MIZIGO YA DAWA ZA KULEVYA YAFICHWA KWENYE MABASI, MITUMBA NA CHAI

 


Dar es Salaam, Januari 08, 2026.

Kufuatia operesheni zilizofanyika mwishoni mwa mwezi Desemba, 2025, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya imekamata kilogamu 9,689.833 za dawa za kulevya, pikipiki kumi na moja na magari matatu. Watuhumiwa 66 wamekamatwa kuhusiana na uhalifu huo.

Katika operesheni iliyofanyika Sinza C mtaa wa Bustani nyumba namba 16, Jefferson Kilonzo Mwende (35), raia wa Kenya, alikamatwa akiwa na gramu 131.88 za heroin. Mtuhumiwa huyo aliyeishi Tanzania tangu 2023, alitumia biashara ya kuuza chai kuficha biashara ya dawa za kulevya anayoifanya.

Aidha, mtaa wa Wailes, Temeke , Dar es Salaam, zilikamatwa pakiti 20 za skanka zenye uzito wa kilogramu 20.03 zikiwa zimefichwa ndani ya balo la mitumba na kufichwa kwenye bus aina ya Scania la kampuni ya King Masai Tours, lenye namba za usajili wa nchi ya Msumbiji namba AAM 297 CA . Bus hilo hufanya safari zake kati ya Nampula nchini Msumbiji na Tanzania. Watuhumiwa waliokamatwa kuhusiana na tukio hilo ni Amasha Iddi Mrisho (40), mkazi wa Buza, Dar es Salaam na Seleman Juma Ally (32), raia wa Msumbiji.

Eneo la Kinyerezi, mtaa wa Majoka wilaya ya Ilala, watuhumiwa Erick Ernest Ndagwa (32), Paul Blass Henry (34), na Tido Emmanuel Mkude (35) walikamatwa wakiwa na bangi kg 193.66, zikisafirishwa kutoka Morogoro kwenda Dar es Salaam.

Kadhalika, kufuatia ukaguzi uliofanyika kwenye kampuni za usafirishaji wa mizigo jijini Dar es Salaam, paketi 20 za dawa za kulevya aina ya mirungi zenye uzito wa kilogramu 9.54 zilikamatwa zikiwa zimefungwa kama majani ya mwarobaini yaliyokaushwa. Dawa hizo zilikuwa zikisafirishwa kutoka Kenya kuelekea Australia.

Vilevile, kupitia operesheni mbalimbali zilifanyika katika mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Morogoro, Tanga, Lindi, Kilimanjaro, Njombe, Kigoma na Arusha zilikamatwa dawa za kulevya aina ya heroin gramu 37.34, skanka kilogramu 1.015, bangi kilogramu 7,969.98 na mirungi kilogramu 1,363.701 pamoja na kuteketeza ekari 14 za mashamba ya bangi.

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya inasisitiza wananchi kutoa taarifa kuhusu viashiria vya biashara ya dawa za kulevya na kuwa makini kutokubali kusafirisha mizigo wasiyoijua. Mamlaka itaendelea na operesheni nchi nzima na kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya wahalifu wa dawa za kulevya.

Imetolewa na; Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali MAMLAKA YA KUDHIBITI NA KUPAMBANA NA DAWA ZA KULEVYA.



















Post a Comment

0 Comments